Sunday, March 11, 2012

HAMMIE RAJAB (SIMU YA KIFO; SANDA YA JAMBAZI; ROHO MKONONI; AMA ZAO AMA ZANGU; TEARS ON VALENTINE DAY)

Mzee Hammie Rajab ameandika vitabu vingi sana vya riwaya na vingine vimetumika mashuleni kwa ajili ya kuwaelimisha wanafunzi wa sekondari na vyuo kama vitabu vya ziada katika somo la fasihi. Ametunga na kuongoza filamu nyingi sana, ambapo nyingine zimetokana na vitabu vyake mwenyewe.

Miongoni mwa vitabu alivyoandika ambavyo bado navikumbuka ni Somo Kaniponza, Gubu la Wifi, Najuta Kuolewa, Sanda ya Jambazi, Ama Zao Ama Zangu, Roho Mkononi, Miujiza ya Mlima Kolelo, Rest in Peace Dear Mother na Ufunguo wa Bandia.

Filamu alizotunga na kuongoza ambazo naweza kuzikumbuka ni Watoto wana Haki, Usawa, Gubu la Wifi, Benki Yako, Miujiza ya Mlima Kolelo, Mama, Kibuyu, Zawadi, Rama, Nawaachieni na Simu ya Kifo.

Hammie Rajab alizaliwa mwaka 1936 mjini Morogoro, akiwa mtoto wa pili katika familia ya marehemu Mzee Rajab Athuman. Jina lake halisi ni Hamisi Rajab Athuman.

Alipata elimu yake ya msingi katika shule ya Msamvu mjini Morogoro, kabla ya kujiunga na Chuo cha Mombasa Institute of Muslim Education (MIOME) nchini Kenya, ambako alisoma kwa miaka mitano na kuhitimu kama fundi makanika kamili.

Baada ya kuhitimu Chuoni, Hammie Rajab alifanyakazi sehemu kadhaa, ikiwemo kampuni ya mafuta (Caltex) mkoani Iringa, Shirika la Reli Tanzania (TRC) na Kampuni ya Filamu Tanzania (TFC), ambako nako aliacha. Baada ya hapo, akaamua kuingia moja kwa moja katika utunzi wa vitabu vya riwaya:
"Alikuwa na uwezo mkubwa sana na amesoma vitabu vingi mno. Hammie alikuwa anaimudu vyema lugha ya Kiingereza, kwa hiyo haikuwa vigumu kwake kuingia katika ulimwengu wa uandishi vitabu," anasema Kassim Rajab Athuman, maarufu kama Wibbo, ambaye ni mdogo wake Hammie Rajab na rafiki yake mkubwa.

Kutokana na gharama kubwa za uchapaji vitabu, zilizosababishwa na ukosefu wa karatasi na soko lenyewe la vitabu, kwa kuwa Watanzania wengi hawana utamaduni wa kujisomea vitabu; kazi ya uandishi na uchapishaji vitabu haikuwa na manufaa makubwa katika miaka ya themanini.

Waandishi wa vitabu, akiwemo Hammie Rajab walikata tamaa na wengi wao wakageukia shughuli zingine za kuendesha maisha yao. Hammie Rajab aligeukia tena ulimwengu wa filamu, ambao alikuwa na uzoefu wa kutosha tangu enzi za TFC.

Katika kipindi cha kuanzia mwaka 1985 mpaka 1995, kulikuwa na wimbi kubwa la mageuzi ya vyombo vya habari nchini, ambapo tulishuhudia vyombo vingi binafsi, kama magazeti, radio na televisheni vikianzishwa, jambo ambalo lilikuwa neema kwa watu wenye vipaji kama Hammie Rajab.

Hammie amewafundisha kazi wafanyakazi wengi tu, wa mwanzo kabisa wa televisheni hapa Tanzania, ambao sasa ni watangazaji maarufu wa radio na televisheni. Wengine ni wahariri na watayarishaji wakubwa wa vipindi vya televisheni.

Huyo ndiyo Hammie Rajab! Si rahisi kumueleza katika kurasa chache za gazeti ukammaliza. Katika fani za utangazaji na filamu, itoshe tu kusema kwamba Hammie alikuwa Encyclopedia!
COURTESY: BISHOPHILUKA Blog

KAZI ZA UTUNZI:
A. VITABU
1. Ama Zao Ama Zangu
2. Simu ya Kifo
3. Sanda ya Jambazi
4. Roho Mkononi
5. Gubu la Wifi
6. Ufunguo wa Bandia.
7. Miujiza ya Mlima Kolelo
8. Somo Kaniponza
9. Najuta Kuolewa
10. Rest in Peace Dear Mother


B. FILAMU
1. SIMU YA KIFO
2. TEARS ON VALENTINE DAY

No comments:

Post a Comment